0
Usajili wa Paul Pogba umevunja rekodi za sajili tano zilizowahi kuwa ghali zaidi duniani baada ya kutua United kwa paundi milioni 89.

Manchester United imethibitisha kukamilisha uhamisho wa kiungo wa Juventus Paul Pogba ambaye amejiunga na mashetani wekundu kwa ada iliyoweka rekodi ya dunia, kwa mujibu wa tovuti rasmi ya Manchester United.

Baada ya uvumi na tetesi za muda mrefu, miamba hiyo ya EPL hatimaye siku ya Jumapili waliujulisha ulimwengu kwamba, dili la Mfaransa huyo kurejea Old Trafford linakaribia kukamilika baada ya kuanza  kwa mchakato wa kumfanyia vipimo vya afya.

Alfajiri ya Jumanne, United walitupia chapisho kwenye mtandao wa twitter kwamba, mchezaji huyo wa zamani wa klabu hiyo amesaini mkataba wa miaka mitano kuitumikia klabu hiyo wenye kipengele cha kuongeza mwaka mmoja zaidi.

Uhamisho huo unatajwa kugharimu £89m, ukivunja rekodi ya usajili ghali zaidi duniani wa £85m uliomshuhudia Gareth Bale akihama kutoka Tottenham Hotspur na kujiunga na Real Madrid mwaka 2013.

Usajili wa Paul Pogba umevunja rekodi ya sajili tano ghali zaidi duniani katika miaka ya hivi karibuni ambapo wachezaji wote walihamia klabu za La Liga, (Hispania), hususani Real Madrid.

Ikumbukwe wachezaji wote hao watano walikuwa wakitoka klabu nyingine kuhamia Real Madrid, Kwa hiyo tangu mwaka 2000-2013, Real Madrid pekee ndiyo klabu iliyosajili wachezaji kwa dau kubwa zaidi duniani rekodi ambayo imevunjwa na Manchester United mwaka 2016.

Mwaka 2000 – Luis Figo £37m (Barcelona kwenda Real Madrid), mwaka 2001 – Zinedine Zidane £46m (Juventus kwenda Real Madrid), mwaka 2009 – Kaka £56m (AC Milan kwenda Real Madrid), 2009 – Cristiano Ronaldo £80m (Manchester United kwenda Real Madrid), 2013 – Gareth Bale £86m (Tottenham Hotspur kwenda Real Madrid)

Chanzo: Goal.com

Post a Comment

 
Top